Home » » NI VIGEZO GANI MAHAKAMA INAZINGATIA KATIKA KUPUNGUZA ADHABU?

NI VIGEZO GANI MAHAKAMA INAZINGATIA KATIKA KUPUNGUZA ADHABU?




Sheria mbali mbali zinazo zungumzia makosa ya jinai hutaja adhabu ambazo mtu anapaswa kupata kutokana na makosa hayo. Adhabu hizi huweza kuwa faini, kifungo, fidia au vyote kwa pamoja.

Endapo mtuhumiwa atakutwa na hatia ya makosa hayo Mheshimiwa hakimu/Jaji anatakiwa kuzingatia sheria inayotoa adhabu hizo pamoja na sheria ya kima cha chini cha hukumu[1] inaelezaje, bila kusahau baadhi ya kanuni kutoka katika kesi zilizo kwisha amuliwa.

Pindi Mtuhumiwa anapopatikana na hatia Mahakama hutoa nafasi kwa muendesha mashtaka kueleza kwa nini Mtuhumiwa apewe adhabu inayostahili kama sheria inavyotaka na pia mahakama itatoa nafasi kwa mtuhumiwa aliyekutwa na hatia kuiomba Mahakama impunguzie adhabu na kwa sababu zipi.

Kifungu cha sita cha sheria ya kima cha chini cha hukumu kinatoa ruhusa kwa Mahakama kutoa hukumu kwa Mtuhumiwa aliyehukumiwa kwa mara ya kwanza kuhukumiwa kanakwamba sheria hiyo haipo, yani kuhukumu vile itakavyoona inafaa.

Kanuni ambazo mahakama inapaswa kuzingatia katika kutoa hukumu zinainishwa katika kesi ya Jamuhuri dhidi Kidato Abdullah[2] ambazo ni uzito wa kosa hilo, rekodi ya mtuhumiwa, umri, maslahi ya jamii ukilinganisha na maslahi ya mtuhumiwa.

Katika kesi ya Jamuhuri dhidi ya Asia Salum na wengine[3]  Jaji Mnzavas alibadili adhabu ya mama na mwanae ambao walikutwa na hatia ya kumpiga mlalamikaji mpaka kumvunja bega la kushoto na kumuumiza usoni hivyo kuhukumiwa miezi kumi na mbili jela, huku adhabu halisi ikiwa ni miaka mitano.

Katika kesi hii Jaji alizingatia kuwa mtoto alikuwa na umri wa miaka 16, alikuwa kidato cha tatu na lilikuwa kosa la kwanza hivyo alimuachia huru akisema kuwa muda aliokuwa amekwisha kaa jela umetosha kama adhabu.

Kwa upande wa mama, Jaji alimuhukumu miezi mitatu badala ya kumi na mbili jela kwa sababu lilikuwa kosa lake la kwanza na hakuwa mkorofi kaika jamii.

Pia katika kesi hii Jji alisema vitu viwili vikuu vya kuzingatia, nanukuu;-
(i)           Pale ambapo mtuhumiwa amekutwa na hatia kwa mara ya kwanza basi mkazo uwekwe katika adhabu ya kumbadilisha, labda tu kosa liwe kubwa kiasi cha kuhitaji kutoa adhabu  ya fundisho au kosa liwe limeenea sana kiasi cha kuhitaji kutoa adhabu ya kuitisha jamii,

(ii)          Mtuhumiwa aliyekutwa na hatia kwa mara ya kwanza hapaswi kupelekwa gerezani ambapo anaweza kujichanganya na wahalifu sugu wa misimu ambao wanaweza mfundisha kuwa muhalifu.

Lakini pia katika Kesi ya Jamuhuri dhidi ya Kabula Mhoja[4] Mahakama kuu ilimuongezea adhabu ya mwaka mmoja jela, Kabula aliyehukumiwa na mahakama ya chini kifungo cha miaka minne
Katika kesi hii Kabula alivunja mikono ya mtoto wa miezi minne kwa kutumia mikono yake. Kabula hakubahatika kupata mtoto kutoka kwa mme wake ambaye alizaa nje ya ndoa na mwanamke mwingine. Hivyo kutokana na kejili za mme wake, kabula siku ya tukio alimtembelea mke mdogo wa mme wake nakuomba kumuona mtoto, alipokabidhiwa mtoto ndipo Kabula alivunja mikono ya mtoto huyo.

Kwa kuzingatia uzito wa kosa Mahakama kuu iliamua kubadilisha adhabu kutoka miaka minne hadi mitano wakati mtuhumiwa alikuwa ameomba apunguziwe adhabu.

Hivyo ni muhimu kutambua kuwa kuna kanuni ambazo mahakama lazima izingatie katika kutoa adhabu, na kanuni hizi zime ainishwa na sheria mbalimbali zinazotaja makosa hayo pamoja na kesi zilizokwisha amuliwa.



[1] The Minimum Sentence Act, Cap, 90, R.E. 2002
[2] R. V. Kidato Abdullah 1973 L.R.T. 82
[3] R. v . Asia Salum and Others 1986 T.L.R. 12
[4] R. v. Kabula Mhoja, 1986 T.L.R. 248

Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. BC LEGAL INFORMER - All Rights Reserved
Template Modify by Creating Website
Proudly powered by Blogger